15th September 2009
Jeshi la Polisi Kisiwa cha Pemba limeanza kutumia maji ya kuwasha kutawanya mamia ya wananchi wanaopinga ubaguzi katika uandikishaji wapiga kura, huku shinikizo la kuzuia zoezi hilo likichukua sura mpya baada ya vyumba vya vituo vya kuandikisha wapigakura kumwagwa upupu.
Miongoni mwa vituo ambako upupu huo umemwagwa, ni pamoja na kwenye skuli ya Shumba Vyamboni, iliyoko katika Jimbo la Tumbe, Wilaya ya Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba.
Kutokana na kitendo hicho, zoezi la uandikishaji wapiga kura lilishindikana kufanyika baada ya maofisa wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) kushindwa kuingia ndani ya vyumba hivyo.
Mkuu wa Kituo hicho, Juma Omari Yusufu, ambaye yeye na maofisa wa ZEC pamoja na vifaa vya kuandikisha wapiga kura walikutwa wakiwa nje ya kituo, alithibitisha upupu huo kumwagwa ndani ya vyumba hivyo.
“Vyumba haviingiliki, kumeingizwa upupu, tumepeleka ripoti kwa wakubwa, tunasubiri maamuzi,” alisema Yusufu.
Mbunge wa Konde, Dk Tarab Ali Tarab (CUF), ambaye ni miongoni mwa waangalizi wa zoezi hilo, alivimba sehemu mbalimbali za mwili wake ikiwamo mikono na uso kutokana na kuathiriwa na upupu huo.
Tangu juzi hakuna hata mtu mmoja aliyejiandikisha katika kituo hicho kutokana na wananchi kugomea zoezi hilo karibu kisiwa chote cha Pemba wakipinga wenzao kukataliwa kuandikishwa baada ya kunyimwa kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi (Zan ID).
Mkurugenzi wa ZEC, Salim Kassim Ali alipoulizwa jana kuhusu hatma ya zoezi hilo, aliahidi kuzungumzia suala hilo baadaye.
Tukio hilo lilitokea saa 6 mchana katika kituo cha Skuli ya Kambini Mchangamdogo, baada ya gari linalotumiwa na kiongozi huyo mmoja wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kisiwani kuwabeba watu hao na kuwapeleka kuandikishwa katika kituo hicho.
Katika tukio hilo, watu kadhaa walijeruhiwa kukimbizwa katika hospitali ya Wilaya ya Wete.
Mbali na hilo askari hao pia walifyatua mabomu ya machozi kuwatawanya wananchi waliokusanyika katika kituo cha Kiuyu Minungwini.
Wakati hayo yakijiri, vurugu kubwa ilitokea kisiwani hapa jana baada ya askari wa Kikosi cha Kuguliza Ghasia (FFU), kutumia maji hayo kuwatawanya wananchi waliojaribu kuwazuia baadhi yao kuandikishwa.
Nayo Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), imesema imeshitushwa na vitendo vinavyoendelea kujitokeza kwa baadhi ya wananchi kugoma kujitokeza kuandikishwa katika daftari la kudumu la wapiga kura.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Kiongozi, Hamza Hassan Juma alitoa kauli hiyo jana baada ya kujitokeza vurugu katika vituo vya uandikishaji wapiga kura na kusababisha mamia ya wananchi kushindwa kujiandikisha katika Kisiwa cha Unguja na Pemba.
CHANZO: NIPASHE